May 27, 2012

ANASWA AKITUHUMIWA KUVUNJA NEEMA CRAFTS IRINGA

Kijana ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja mkazi wa kata ya Makorongoni mjini Iringa akiwa amewekwa chini ya ulinzi baada ya kukutwa akivunja eneo la ofisi za Neema Crafts mjini Iringa jana usiku (picha na Jeremia Chaula Photo wa www.blogspot.com)
Hapa akiadhibiwa kwa kumwagiwa maji ya baridi
Jamani wadau anafahamika huyo?
Vijana hawa wanadaiwa kuwa kundi la vijana zaidi ya wanne na baada ya kukurupushwa na walinzi walikimbia na kumsahau mwenzao huyo ambaye aliwekewa mtigo na walinzi wa eneo hilo ,nyuma yake ni eneo ambalo walianza kulivunja kulia

BREAKINGNEWS.....RAIA WA INDIA ADAIWA KUNYANYASA WANAWAKE IRINGA ANAMILIKI MAHABUSU BINAFSI ,POLISI WAMSAKA

Mwanamke Edna Panzi (47) akiwa mahabusu katika ofisi za b\Barc zinazomilikiwa na raia huyo wa India zipo eneo la Ilala mjini Iringa
Polisi wakimhoji mwanamke huyo akiwa katika mahabusu
Wananchi wakiwa wameizunguka ofisi hiyo ya Brac eneo la Ilala mjini Iringa


Naibu meya wa Manispaa ya Iringa Grevas Ndaki akiungana na wananchi wake kushuhudia unyanyasaji wa raia huyo wa India dhidi ya wanawake

Polisi wakiwa wamefanikiwa kumtoa mahabusu mwanamke huyo

JESHI la polisi mkoani Iringa linamsaka mkurugenzi wa taasisi ya mikopo ya Brac ambaye ni Raia wa India kwa tuhuma za kumnyanyasa kwa kumfungia katika mahabusu binafsi ofisini kwake mwanamke mmoja Edina Panzi (47) mkazi wa Ilala katika Manispaa ya Iringa akimdai kiasi cha shilingi 5800 .

Kaimu kamanda wa polisi wa mkoa wa Iringa Peter Kakamba alisema kuwa raia huyo wa India anasakwa na jeshi la polisi mkoani Iringa baada ya kumfungia katika mahabusu mwanamke huyo ambaye alikopeshwa fedha na taasisi yake hiyo ya Brac tawi la Ilala mjini Iringa.

Bila kumtaja jina raia huyo wa India ,kamanda Kakamba alisema kuwa tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 11 jioni katika eneo la Ilala ambako zipo ofisi za taasisi hiyo ya Brac baada ya jeshi la polisi kupata taarifa kutoka kwa rai wema kuhusiana na mwanamke huyo kufungia katika mahabusu katika ofisi hiyo kabla ya polisi kufika kumfungulia mlango mwanamke huyo.

"Jeshi la polisi lilipata taarifa kutoka kwa wasamaria wema kuhusuana na mwanamke huyo kufungia katika mahabusu hiyo kwa sababu ambavyo raia huyo wa India anazijua yeye na ndipo polisi walipofika na kufanikiwa kufungua mahabusu hiyo na kumtoa mwamamke huyo "

Kakamba alisema kuwa taasisi hiyo imekuwa ikijishughulisha na utoaji wa mikopo kwa wanawake jambo ambalo si baya ila ubaya unakuja pale ambapo mkopeshaji huyo anajichukulia sheria mkononi kwa kutoa adhabu iliyo kinyume na sheria za nchi hii kwa kuwafungia mahabusu wakopaji wake.

Kwani alisema kuwa haipo sheria inayomruhusu mtu awaye yeyote yule ama taasisi ya ulinzi kumiliki mahabusu kwa kukamata watu na kuwafungia mahabusu kwani kufanya hivyo ni kosa na wanapatikana na tuhuma kama hizo wakikamatwa hufikishwa mahakamani.

Hivyo alisema kuwa jeshi la polisi linaendesha msako mkali wa kumsaka mkurugenzi huyo wa Brac ambaye ni rai wa India ili kufikishwa mahakamani .

Kwa upande wake mwanamke huyo anayedaiwa kufungiwa mahabusu alisema kuwa alifungiwa katika mahabusu hiyo juzi kuanzia majira ya saa 4 asubuhi hadi saa 11 jioni kabla ya waandishi wa habari wa mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP) kuweza kufika eneo hilo na kutoa taarifa hiyo polisi .

Mwanamke huyo alisema kuwa jumla ya deni lote alilokopa lilikuwa ni kiasi cha shilingi 500,000 na hadi anakamatwa na kufungiwa katika mahabusu hiyo alikuwa akidaiwa kiasi cha shilingi 5800 pekee .

Diwani wa kata hiyo ya Ilala ambaye pia ni naibu meya wa Manispaa ya Iringa Grevas Ndaki alisema kuwa uongozi wa kata hiyo hauungi mkono hata kidogo unyanyasaji unaofanywa na Raia huyo wa India kwa wanawake wa kata hiyo na kuwa kutokana na tabia hiyo kuendelea kuchukua kasi wanaona ni vema ofisi hiyo kuondolewa katika kata hiyo .

TAARIFA KUTOKA TFF LEO


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Mei 27, 2012
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ilikutana Mei 26 mwaka huu ili kutoa mwongozo wa nini kifanyike ndani ya Yanga baada ya wajumbe wake kudhaa kujiuzulu. Kamati ya Uchaguzi ya Yanga ilikuwa imeomba mwongozo huo TFF.
Baada ya kupata taarifa rasmi kutoka Yanga, Kamati imebaini kuwa Kamati ya Utendaji ya Yanga imekosa akidi baada ya wajumbe wake wengi kujiuzulu hivyo kutokuwa na uwezo wa kufanya uamuzi kwa mujibu wa Ibara ya 32(1) ya Katiba ya klabu hiyo.
Hivyo, Kamati imetoa mwongozo kwa Kamati ya Uchaguzi ya TFF ambayo ndiyo msimamizi wa Kamati ya Uchaguzi ya Yanga kuwa ili Kamati ya Utendaji ya Yanga iwe na nguvu za kikatiba kufanya shughuli zake ikiwemo uamuzi wa masuala mbalimbali ndani ya klabu hiyo ni lazima iwe na akidi.
Kwa mujibu wa Ibara ya 29(3) ya Katiba ya Yanga nafasi zilizo wazi katika Kamati ya Utendaji zinatakiwa kujazwa katika Mkutano Mkuu wa Kawaida ujao.
Pia Kamati imebaini uteuzi wa kujaza nafasi zilizo wazi za wajumbe uliofanywa na Kamati ya Utendaji ya Yanga, Mei 21 mwaka huu ni batili kwa vile Kamati ya Utendaji iliyofanya uteuzi huo haikuwa na akidi.
Ili kupata akidi na kufanya uamuzi Kamati ya Utendaji ya Yanga yenye wajumbe 13 inatakiwa kuwa na asilimia 50 ya wajumbe wote, hivyo ili wafanye uamuzi halali hawatakiwi kupungua saba.
Kwa wajumbe ambao hawajajiuzulu; Sarah Ramadhan, Mohamed Bhinda, Tito Osoro na Salim Rupia kwa sasa hawawezi kufanya shughuli zozote za Yanga hadi nafasi zilizo wazi katika Kamati ya Utendaji zitakapojazwa.
Kama inavyoelekeza Katiba ya Yanga, shughuli za kila siku za klabu hiyo zitaendelea kufanywa na Sekretarieti ya Yanga ambayo kiongozi wake ni Katibu Mkuu.
Alex Mgongolwa
Mwenyekiti
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji

KAMPUNI YA SIMU YA AIRTEL YAMUUNGANO MKONO MBUNGE PROF MSOLLA JIMBONI

Mbunge wa jimbo la Kilolo ,Prof Peter Msolla (kulia) akikabidhi msaada wa kompyuta tatu na vitabu vilivyotolewa na kampuni ya simu ya artel vyote vikiwa na thamani ya Tsh.milioni 9 kushoto ni mwakilishi wa artel mkoa wa Iringa ,Hildegrad Ntamuturano

MBUNGE wa jimbo la Kilolo mkoani Iringa Profesa Peter Msolla amekabidhi msaada wa kompyuta tatu na vitabu vya kiada msaada wenye thamani ya shilingi milioni 9 uliotolewa na kampuni ya simu ya airtel katika shule tatu za sekondari jimboni kwake .

Akikabidhi msaada huo katika hafla fupi iliyofanyika katika viwanja vya shule ya Sekondari Mazombe juzi ,Prof.Msolla alisema kuwa msaada huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zake katika kuendeleza elimu kwa wananchi wake.

Prof Msolla alisema kuwa mbali ya kuwa shule hiyo ya sekondari Mazombe haina umeme ila ametanguliza kompyuta hizo kama njia ya kuanza mkakati wa kuisaidia shule hiyo kupata umeme wa mionzi ya juu ,umeme ambao atasaidia kuufunga katika shule hiyo.

Alisema kuwa shule hiyo ilikuwa ikikabiliwa na tatizo la kompyuta na kupelekea walimu kushindwa kuchapa mitihani ama kuandaa masomo yao kwa kutumia kompyuta na kuishia kuandaa mitihani na vipindi mbali mbali kwa kuandika kwa mkono jambo ambalo lilikuwa likikwamisha shughuli mbali mbali shuleni hapo.

Mbunge Prof Msolla alisema msaada huo wa kompyuta na vitabu vya kiada katika shule hiyo na shule ya Sekondari Maria Consolata , Udzungwa na Mazombe umetolewa na kampuni ya simu ya airtel Tanzania .

"Napenda kulipongeza sana kampuni ya simu ya airtel kwa kusaidia maendeleo ya elimu katika jimbo langu .....ndugu zangu wanafunzi na wazazi moja kati ya vipaumbele vyangu vilikuwa ni elimu na wakati nikiingia madarakani mwaka 2005 Kilolo ilikuwa na shule za sekondari tatu ila sasa tumepiga hatua na kuwa na shule zaidi ya 20 ....napenda kuwahakikishieni kuwa tutaendelea kupiga hatua katika maendeleo ya elimu "

Pia aliwataka wanafunzi kutumia vizuri nafasi hiyo waliyoipata kwa kuendelea kusoma kwa juhudi kubwa na kuwa katika dunia ya sasa elimu ndio kila kitu na bila elimu ni vigumu kuweza kufanikiwa .

Awali mwakilishi wa artel mkoa wa Iringa Bi Hildegrad Ntamuturano alisema kuwa kampuni yake imeendelea kusaidia jamii katika mambo mbali mbali na kuwa mbali ya msaada huo wa vitabu na kompyuta bado wataendelea kusaidia katika maeneo mengine ya kijamii hapa nchini .

Akishukuru kwa msaada huo kwa niaba ya walimu wakuu wenzake mkuu wa shule ya sekondari Maria Consolata Bw. Mufwalamagoha Kibasa alisema kuwa jitihada zinazofanywa na mbunge Prof Msolla katika jimbo hilo ni mfano wa kuigwa kwa wabunge wengine na kuwa kati ya vitu vizuri ambavyo wabunge wanapaswa kutambua ni elimu hivyo ni vema kuelekeza nguvu zao katika kusaidia elimu.

ZITTO KABWE ASEMA MAFUTA KUWA SUALA LA MUUNGANO NI KOSA

Mhe.Zitto Kabwe (mb)
  • Kila upande wa Muungano uchimbe Mafuta na Gesi Asili yake na Mapato yawe ya Serikali ya upande husika.
  • Shughuli za Utafutaji kwenye vitalu vyenye mgogoro ziendelee mara moja
  • Zanzibar ianzishe Shirika lake la Mafuta (PetroZan)
  • Katiba mpya itofautishe utafutaji (upstream) na Biashara (uchimbaji, midstream na downstream)
Moja ya suala linalosubiriwa kwa hamu kubwa katika mjadala na hatimaye uandishi wa Katiba mpya ni suala la Mafuta na Gesi Asilia kuwa jambo la Muungano au liondolewe katika orodha ya mambo ya Muungano. Suala hili limezusha mjadala mkubwa sana mara kwa mara nchini Tanzania kiasi cha lenyewe kuwa ni hoja ya wale wasiotaka tuwe na Dola ya Jamhuri ya Muungano Tanzania.
Wakati Muungano unaanzishwa mwaka 1964 Mafuta na Gesi hayakuwa masuala ya Muungano. Nimeangalia katika Hati ya Muungano ambayo ilikuwa ni sehemu ya Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1965, suala hili halikuwamo katika orodha ya mambo Kumi na Moja ya Muungano. Nyaraka nilizoziona zinaonyesha kwamba suala la Mafuta na Gesi Asilia liliongezwa katika orodha ya Mambo ya Muungano mwaka 1968. Kuna watu wanahoji kihalali kabisa kwamba nyongeza ya jambo hili ilifanywa bila kufuata taratibu na hivyo kufanywa kinyemela na kuna wengine wanasema jambo hili lilifuata taratibu zote za kisheria ikiwemo kupigiwa kura na Bunge la Muungano na kuungwa mkono na theluthi mbili ya Wabunge kutoka pande zote za Muungano.
Katika moja ya vikao vya Bunge katika Bunge la Tisa, aliyekuwa Naibu wa Waziri wa Nishati na Madini Ndugu Adam Malima alileta kumbukumbu za mjadala Bungeni (Hansard) za mjadala wa suala la Mafuta na Gesi ili kuthibitisha kwamba jambo hili halikuuingizwa kwenye Katiba kinyemela.
Wakati umefika kwa Watafiti wa Masuala ya Muungano wakapekua nyaraka hizi na kutwambia ukweli ulio ukweli mtupu wa namna suala la Mafuta na Gesi lilivyoingizwa katika orodha ya mambo ya Muungano. Hata hivyo, jambo hili sasa ni jambo la Muungano kwa mujibu wa Katiba na ni dhahiri kuwa WaTanzania wa Zanzibar hawafurahiswhi nalo na hivyo kuazimia kupitia Azimio la Baraza la Wawakilishi kwamba jambo hili liondolewe kwenye orodha ya masuala ya Muungano. Kwa vyovote vile Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inapaswa kutoa uamuzi wa mwisho utakaomaliza mjadala huu.
Jambo la kusikitisha ni kwamba licha ya Bunge la Muungano kuamua kuongeza suala la Mafuta na Gesi asilia katika masuala ya Muungano, mwaka mmoja baada ya uamuzi huo likaundwa Shirika la Maendeleo ya Mafuta Tanzania (TPDC) kwa amri ya Rais wa Jamhuri ya Muungano (establishment order). Shirika hili halikuanzishwa kwa Sheria ya Bunge au kwa Sheria ya Makampuni kama yalivyo Mashirika mengi ya Umma hapa nchini bali kwa amri ya Rais ya mwaka 1960. Katika amri hii ya Rais, Shirika la TPDC halikupewa ‘mandate’ ya kimuungano. Shirika hili mipaka yake ilianishwa kuwa ni Tanzania bara peke yake. Hivyo suala la Muungano likawekewa Shirika la Tanganyika kulisimamia!
Kama ilikuwa ni bahati mbaya au makusudi au kupitiwa kwa viongozi wetu wa wakati huo ni vigumu kujua lakini huu ni mkanganyiko mkubwa ambao ulipaswa kurekebishwa mapema sana.
Shirika la TPDC limekuwa likifanya kazi ya kusimamia Sekta ya Mafuta na Gesi ikiwemo kutoa vibali vya kutafuta mafuta, kuingia mikataba na Makampuni ya kimataifa na kuisimamia mikataba hiyo. Miongoni mwa mikataba hiyo ni kwenye maeneo ambayo kama isingekuwa Muungano yangekuwa ni Maeneo ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Mbaya zaidi Mikataba yote ya utafutaji na uchimbaji Mafuta inafanywa inaingiwa na Waziri wa Nishati na Madini Wizara ambayo sio ya Muungano. Hakuna hata eneo moja ambalo taratibu zimewekwa kwamba pale ambapo eneo hilo ni eneo lilikuwa chini ya himaya ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar basi mikataba isainiwe na Mawaziri wawili wa sekta hiyo kutoka kila upande wa Muungano.
Ni dhahiri kwamba kama ni kusahau hapa kulikuwa na kusahau kukubwa ambako hakustahmiliki kwa mtu yeyote mwenye upeo achilia mbali mwananchi wa kawaida wa Zanzibar ambaye anaona anaonewa na kugandamizwa na Bara.
Mnamo miaka ya mwanzo ya 2000, Shirika la TPDC liliingia mikataba ya Vitalu kadhaa vya Mafuta miongoni vya vitalu hivyo ni vitalu nambari 9, 10, 11 na 12 mashariki ya visiwa vya Pemba na Unguja. Vile vile Shirika na Wizara ya Nishati waliingia mkataba mwingine katika Kitalu kilichopo kati ya Pemba na Tanga (mahala ambapo kumekuwa na dalili za wazi za kuwapo Mafuta kutokana na kuonekana kwa ‘Oil sips’ mara kwa mara.
Vitalu 9, 10, 11 na 12 vilipewa kampuni ya Shell ya Uholanzi na kitalu cha kati ya Tanga na Pemba walipewa Kampuni ya Antrim ya Canada ambayo baadaye waliuza sehemu ya Kampuni yao kwa Kampuni ya RAK Gas kutoka Ras Al Khaimah huko United Aarab Emirates. Kwa kuwa Vitalu hivi vipo katika eneo la iliyokuwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kabla ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilikataa shughuli zozote kufanyika mpaka suala la Mafuta na Gesi kuondolewa katika orodha ya Mambo ya Muungano lipatiwe ufumbuzi.
Uamuzi huu wa Serikali ya Zanzibar ni uamuzi ambao ungechukuliwa na Serikali yeyote ile yenye mapenzi ya dhati na watu wake. Uamuzi huu ulileta mjadala mpana sana katika masuala ya Muungano na ambao hawana taarifa waliubeza sana. Hata hivyo suala hili likafanywa ajenda katika vikao vya masuala ya Muungano vinavyoitwa Vikao vya Kero za Muungano. Miaka kumi suala hili linajadiliwa na Maamuzi hayafanyiki! Hivi sasa kila suala lenye kuangukia kwenye Katiba husukumwa huko na hivyo kutoa ahueni kwa wanaogopa kufanya maamuzi.
Katika medani za uchumi kila suala lina muda wake. Masuala ya utafutaji wa Mafuta ni masuala yanayoongozwa na msimu na kuendelea kuchelewa kufanya maamuzi juu ya suala hili kunalitia hasara Taifa, Hasara ya Mabilioni ya Fedha na hasara kubwa zaidi ya kufahamu utajiri uliojificha chini ya Maji ya Bahari inayozunguka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hivi sasa Pwani ya Afrika Mashariki inarindima (trending) katika utafutaji wa Mafuta na Gesi asilia. Huko Msumbiji Makampuni mbalimbali yamegundua Gesi asilia nyingi inayofikia zaidi ya futi za ujazo trillion 107 (107TCF) kwa makadirio ya chini. Hapa Tanzania utajiri wa Gesi asilia uliogunduliwa hadi hivi sasa na kutangazwa umefikia futi za ujazo trillion 20 (20TCF) ambazo ni sawa na utajiri wa thamani ya dola za kimarekani trillion 6. Makadirio yanakisiwa kuwa Tanzania kuna futi za ujazo trillioni 85 (85TCF) za Gesi Asilia katika eneo la Kusini kuanzia vitalu namba 1 mpaka namba 5 ikiwemo vitalu vya nchi kavu na vile vya Songosongo.
Iwapo kasi ya utafutaji mafuta itaendelea kama sasa katika kipindi cha miaka 2 ijayo Tanzania itaweza kuwa kati ya nchi mbili za Afrika zenye Utajiri mwingi zaidi wa Gesi Asilia. Hivi sasa Nigeria ndio inaongoza kwa kuwa na futi za ujazo trillion 189 (189TCF) ikifuatiwa na Algeria na Angola ambazo zote zina utajiri wa juu kidogo ya 100TCF kwa Algeria na chini ya 100TCF kwa Angola. Msumbiji sasa imeifikia Algeria na kushika nafasi ya pili.
Katika masuala ya Mafuta na Gesi hatua ya kwanza ni kujua kama utajiri huu ambayo kitaalamu inaitwa gas exploration. Shughuli za utafutaji zinapandisha sana thamani ya nchi na eneo la nchi. Kwa mfano hivi sasa kitendo cha Kampuni ya Uingereza ya BG/Ophir na ile ya Norway ya StatOil kupata mafanikio makubwa katika utafutaji wa Gesi asilia kumeongeza thamani ya Pwani ya kusini ya Tanzania katika medani za utafutaji (Exploration Activities).
Hata hivyo kama ilivyogusiwa hapo juu, shughuli za Utafutaji ni shughuli za msimu. Pia huchukua muda mrefu wa kati ya miaka 5 mpaka 10 kati ya kutafuta, kupata na kuanza kuchimba. Hivi sasa ni muda wa pwani ya Afrika Mashariki. Ni lazima kuhakikisha kwamba vitalu vyote vilivyogawiwa hivi sasa vinafanyiwa kazi. Hata hivyo vitalu vingine vyovyote visigawiwe kwanza mpaka hapo matunda ya vitalu vya sasa yaonekane. Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini imependekeza kusimamisha kugawa vitalu vipya. Matokeo ya utafutaji katika vitalu vya sasa yakiwa mazuri kama ilivyo sasa, thamani ya vitalu vipya itapanda sana na nchi itakuwa na nguvu ya majadiliano (strong negotiation position) dhidi ya makampuni makubwa ya mafuta.
Tufanyaje kuhusu vitalu vilivyogawiwa katika eneo ambalo lina mgogoro kuhusu suala la Muungano? Sio kazi rahisi lakini imefikia wakati tuamue. Kwa kadri nionavyo, Itabidi kuwe na maamuzi ya mpito (interim decisions) na maamuzi ya muda mrefu.
Kwanza, ni lazima kukiri tulipokosea. Hata kama ilikuwa ni sahihi kiutaratibu kuweka suala la mafuta na Gesi katika orodha ya mambo ya Muungano, haikuwa halali Shirika la TPDC lenye mipaka ndani ya Tanzania bara kuingilia ugawaji wa vitalu na kuingia mikataba katika maeneo ambayo ni ya Muungano. Ni Taasisi ya Muungano tu ndio inaweza kushughulikia suala la Muungano na sio vinginevyo.
Ilikuwa ni dharau kubwa sana kwa Waziri wa Nishati ambayo sio Wizara ya Muungano kuingia Mikataba katika eneo la Zanzibar (ambapo kikatiba tumelifanya eneo la Muungano) bila kushauriana na kukubaliana na Waziri wa Nishati wa Zanzibar. Kukiri kosa sio unyonge, ni uungwana. Hata tukifanya vikao milioni moja chini ya Makamu wa Rais, bila kukiri kosa hili tatizo hili na mengine ya aina hii hayataisha.
Pili, ni vema kukubali kwamba shughuli za utafutaji katika vitalu vyenye mgogoro ziendelee kwenye hatua ya utafutaji tu. Kama mafuta au Gesi ikipatikana, uchimbaji usianze mpaka uamuzi wa mwisho kuhusu suala hili uwe umepatikana. Pia ninapendekeza ufumbuzi wa mwisho hapa chini. Kuchelewesha utafutaji ni hasara kwa pande zote za Muungano kutokana na taarifa za kijiolojia zitakazopatikana na hivyo kupandisha thamani ya nchi hizi mbili kijiolojia.
Hata hivyo, utafutaji huu katika eneo lenye mgogoro kati ya pande mbili za Muungano ufanyike baada ya mkataba wa PSA kufanyiwa marekebisho makubwa. Marekebisho hayo ni pamoja na Mkataba kusema wazi kwamba shughuli za uchimbaji zitafanyika iwapo tu makubaliano ya kugawana mapato ya Mafuta na Gesi kati ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar yamefikiwa. Pia Mkataba uzingatie maendeleo ya sasa ya kusini mwa Tanzania na hivyo mkataba uboreshwe kwa faida ya nchi ikiwemo kutolewa kwa ‘signature bonus’. Hii ni Fedha inayotolewa na Kampuni za utafutaji Mafuta kwa Serikali kabla ya utafutaji kuanza. Kiwango hutokana na majadiliano na kukubaliana. Nchi zenye jiolojia iliyopevuka hutumia njia hii kuongeza mapato ya Serikali.
Mkataba pia useme kinaga ubaga kwamba utasainiwa na Mawaziri wa pande mbili za Muungano na kwamba Kampuni inayofanya utafiti itatoa taarifa zake za Utafiti sawia kwa Mawaziri wote kwa mujibu wa vipengele vya mkataba.
Kwa upande wa maamuzi ya muda mrefu, ushauri wangu ni kwamba; kwa maana ya kuandikwa kwenye Katiba mpya ni kwamba Suala la Mafuta na Gesi Asilia liendelee kuwa suala la Muungano kwenye eneo la usimamizi wa Tasnia na leseni za utafutaji (Upstream Regulatory mechanism). Hili ni eneo linalohitaji usimamizi wa dhati kabisa na kwa pamoja pande mbili za Muungano zinaweza kufanya vizuri zaidi.
Eneo la Uchimbaji na hasa kugawana mapato ya mafuta na Gesi (Profit Oil) lisimamiwe na kila upande wa Muungano kivyake. Biashara ya Mafuta isiwe jambo la Muungano na hivyo kila Upande wa Muungano uwe na Shirika lake la Mafuta na Gesi ambalo litashiriki kama mbia wa Mashirika ya Kimataifa katika uchimbaji, usafirishaji na uuzaji wa Mafuta na Gesi Asilia. Mapato yanayotokana na Mafuta (Profit Oil) na kodi nyingine zote isipokuwa mrahaba (royalty) yawe ni masuala yanayoshughulikiwa na Serikali ya kila upande wa Muungano kwa mujibu wa Sheria ambayo Serikali hizo zimejiwekea.
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ilipendekeza Bungeni kwamba kuwepo na Mamlaka ya Mafuta na Gesi Asilia Tanzania (Tanzania Petroleum Authority) ambayo itakuwa ni msimamizi (upstream regulator) kama suala la Muungano. Mrahaba wa Mafuta na Gesi ambao sasa ni asilimia 12 ya Mapato ya Mafuta itakusanywa na Msimamizi huyu na ndio mapato pekee katika tasnia ya Mafuta na Gesi yanapaswa kuwa mapato ya Serikali ya Muungano.
Kamati pia ilipendekeza kuanzishwa kwa Shirika la Mafuta na Gesi (Petroleum Tanzania - PetroTan) ambalo litakuwa mbia kwenye Makampuni ya utafutaji na uchimbaji wa Mafuta na Gesi kwenye Vitalu vya Tanzania bara. Mapato yote ya vitalu vya Tanzania bara na kodi zote isipokuwa Mrahaba zitakwenda kwa Mamlaka za bara tutakazo kuwa tumeamua baada ya Katiba mpya kuanza kazi. Hivi sasa TPDC inafanya kazi hii mpaka Zanzibar jambo ambalo hata kwa akili ya kawaida halipaswi kukubalika.
Aidha, napendekeza kwamba Zanzibar ianzishe Shirika lake la Mafuta sasa. Jambo hili halina haja ya kusubiri vikao vya kero za Muungano kwani ni dhahiri TPDC haina mamlaka,ushawishi na uthubutu kusema uhalali wa kusimamia vitalu vya Mafuta vilivyopo Zanzibar.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipeleke muswada katika Baraza la Wawakilishi kuanzisha Shirika la Mafuta na Gesi la Zanzibar (Petroleum Corporation of Zanzibar – PetroZan) ili liweze kushiriki katika utafutaji na uchimbaji wa Mafuta Zanzibar. Lakini Pia PetroZan ilinde maslahi ya Zanzibar katika tasnia hii kwa kujijengea uwezo wa kusimamia ugawaji bora wa Mapato kutoka katika Mafuta na Gesi Asilia.
Kama Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inachelea kuanzishwa kwa Shirika hili, Wawakilishi wa pande zote (CCM na CUF) wapeleke muswada binafsi kuunda Shirika la Mafuta la Wazanzibari. Hawatakuwa wamevunja Katiba ya Muungano kwani hivi sasa hakuna Taasisi yenye mamlaka ya kusimamia Tasnia hii kwa Upande wa Zanzibar.
Wakati haya yote yanafanyika, shughuli za utafutaji Mafuta na Gesi katika vitalu vilivyopo katika eneo la Zanzibar na hasa vitalu namba 9,10,11 na 12 na katika kitalu cha kati ya Pemba na Tanga ziendelee kufuatia marekebisho ya Mkataba wa Utafutaji. Utafutaji wa Mafuta una faida zaidi kwa Nchi hizi mbili kuliko kwa Kampuni za Mafuta kwani uwekezaji wa Kampuni pekee na nchi zitapata taarifa za kijiolojia zitakazosaidia mikataba ya baadaye kuwa bora zaidi.
Wakati nasisitiza kwamba tuendelee na utafutaji katika vitalu tajwa, katika Katiba mpya, utafutaji wa mafuta usimamiwe na Taasisi ya Muungano. Uchimbaji na biashara ya Mafuta ufanywe na kila Serikali ya kila upande wa Muungano. Mafuta kuwa jambo la Muungano halafu kusimamiwa na Shirika la Tanganyika na Wizara ya Upande mmoja ya Muungano ndio chanzo cha mgogoro. Suluhisho sio kuifanya TPDC kuwa Shirika la Muungano, bali kila upande upewe uhuru wa kusimamia uchimbaji, Biashara na mlolongo mzima wa tasnia ya Mafuta (value chain from midstream to downstream) isipokuwa utafutaji (upstream). Hili ndio suluhisho la kudumu ninaloona linafaa.
Uwazi (declaration):
Zitto Kabwe ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini na mfuatiliaji wa karibu wa Tasnia ya Mafuta na Gesi Asilia akiwa amesomea mfumo wa uchumi wa katika tasnia ya madini na mafuta (fiscal regime in Mineral and Petroleum sector). Zitto pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ambayo inasimamia mahesabu na utendaji wa Shirika la TPDC. Makala hii imeandikwa baada ya ziara ya Mafunzo ya Wabunge kutembelea nchi ya Uholanzi kwa ufadhili wa Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo. Katika ziara hiyo Wabunge hao walikutana na Wakuu wa Shirika la Mafuta la Shell ambapo walizungumzia pia suala la vitalu namba 9, 10, 11 na 12.

May 26, 2012

MISS DAR INTER COLLEGE KURINDIMA JUNI 8 CLUB SUNCIRO

SHINDANO la kumsaka Miss Dar Intercollege 2012 linatarajiwa kufanyika Juni 8 kwenye ukumbi wa Sunciro, ulipo Sinza Shekilango jijini Dar es Salaam, imefahamika.

Mratibu wa Shindano hilo Dina Ismail alisema jana kwamba warembo watakaoshiriki shindano hilo wanaendeleza na mazoezi kwenye hoteli ya Lamada jijini Dar es Salaam chini ya ukufunzi wa Marylidya Boniface, huku kwa upande wa shoo wakinolewa na Bob Rich.

Alisema mpaka sasa warembo 12 kutoka vyuo vya Biashara (CBE), Uandishi wa Habari (DSJ) na Time, Ustawi wa Jamii na kile cha Usimamizi wa Fedha (IFM) wamesharipoti kambini.

Dina aliwataja warembo hao kuwa ni pamoja na Hilda Edward, Nancy Maganga, Saada Seleman, Neema Nashon, Rose Muchunguzi, Fina Revocatus,Jane Augustino,Theresia Issaya na Natasha Deo.Taji la kitongoji hicho linashikiliwa na Rose Msuya kutoka IFM.

Kwa upande mwingine, mratibu huyo ameyaomba makampuni mbalimbali kujitokeza kudhamini shindano hilo ambalo linatarajiwa kuwa la aina yake na hasa ikizingatiwa kuwa washiriki wake wana vigezo vya hali ya juu.

“Tunaomba makampuni mbalimbali yajitokeze kudhamini shindano letu…mpaka sasa wadhamini tulionao ni pamoja na kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia bia ya Redd’s, Lamada Hotel, Ndege Insurance, Dodoma Wine na Clouds Fm

HAPPY BATHIDAY YA AMINA SHAMTE YATIKISA IRINGA

Amina Shamte akimlisha keki rafiki yake Hildegrad Ntumutaruno wa airtel Iringa wakati wa sherehe yake ya kuzaliwa jana
Amina Shamte akiwashukuru marafiki zake waliofika kusherekea siku yake ya kuzaliwa
Baada ya msosi na vinywa wadau wakicheza muziki

















TULLO CHAMBO AULA TASWA


CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) kinatoa pongezi kwa Mhariri wa Habari za Michezo wa gazeti la Tanzania Daima, Tullo Chambo kwa kuchaguliwa kuwa Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Chama cha Riadha Tanzania (RT).

Chambo alitwaa nafasi hiyo kwenye Uchaguzi Mkuu wa RT uliofanyika Jumapili mjini Morogoro, ambapo ni miongoni mwa wajumbe wapya walioingia kwenye chama hicho.

Wengine walioshinda ni Anthony Mtaka ambaye anakuwa Rais mpya wa RT, wakati Makamu wa Rais Utawala ni William Kallaghe, Makamu wa Rais Ufundi, Dk. Ahmed Ndee, Katibu Mkuu, Suleiman Nyambui, Katibu Msaidizi, Ombeni Zavalla, Mhazini, Is-Haq Suleiman.

Wajumbe wa Kamati ya Utendaji ni Mwinga Mwanjala, Meta Petro, Peter Mwita, Rehema Killo, Lwiza John, Zakaria Barrie, Zakaria Gwanda, Robert Kalyahe na Christian Matembo.

TASWA inatambua Chambo ni mwanahabari mzoefu, ambaye kwa muda mrefu amekuwa mhariri wa habari za michezo na ni mtu mwenye kujua mambo mengi yanayohusu riadha, hivyo atakuwa kiungo muhimu kwa watu wa riadha, pia atakuwa kiongo kizuri kwa waandishi wa habari za michezo kuhusiana na mambo ya riadha.

TASWA inaahidi kumpa ushirikiano wa kutosha kadri itakavyoweza na inamtakia kila la heri, huku ikiamini hatawaangusha Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa RT waliomuamini wakamchagua kushika wadhifa huo.

Pia Taswa inawapongeza viongozi wote wa RT walioingia madarakani Jumapili, ikiamini watakuwa chachu ya mafanikio ya riadha hapa nchini.

Nawasilisha.

Amir Mhando

Katibu Mkuu TASWA

25/05/2012

WANANCHI RUAHA MBUYUNI WADAI WAMEKUWA WAKIUZIWA MAJI YA MTO

Wananchi wa tarafa ya Mahenge katika wilaya ya Kilolo wakiwa katika mdahalo leo
mwakilishi wa mkurugenzi wa Kilolo John Kiteve akijibu maswali katika mdahalo huo ambao ulipaswa pia kuhudhuria na mbunge wa jimbo la Kilolo Prof.Peter Msolla
Wanawake wa Kilolo wakiwa katika mdahalo huo leo

Wananchi wa Ruaha mbuyuni jimbo la Kilolo mkoani wamelalamikia hatua ya uongozi wa kijiji hicho kuwauzia maji wanayochota katika mto Ruaha jambo ambalo wamedai kuwa ni sawa na unyanyasaji .

Wakizungumza katika mdahalo ulioandaliwa na azaki za kiraia mkoa wa Iringa mdahalo ulioendeshwa na asasi ya Isico katika ukumbi wa Upendo Ruaha Mbuyuni leo .

Wananchi hao wamesema kuwa wanashangazwa na ufisadi unaofanywa na viongozi wa kijiji hicho kwa kuwauzia ndoo moja ya maji wanayochota katika mto Ruah kiasi cha shilingi 200 jambo ambalo wao wanalifananisha na ufisadi na unyanyasaji mkubwa.

Hivyo walihoji sababu ya uongozi wa kijiji hicho kuwauzia maji ambayo si ya bomba ni maji yanayochota katika mto .

Kutokana na hali hiyo wameiomba asasi hiyo ya Isico kufikisha kilio chao hicho kwa mbunge wao Prof Peter Msolla ambaye alipaswa kushiriki katika mdahalo huo ,ili kuweza kuangalia uwezekano wa kuchimbiwa kisima cha maji safi kutokana na maji wanayotumia sasa kutoka katika mto huo kutokuwa safi na salama.

Mwakilishi wa mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo Bw John Kiteve alitaka suala hilo kuweza kuangalia na kuwa si haki kwa kijiji kuwatoza wananchi maji ya mto ambayo .